AVDelta News
Skip to main content Skip to page footer

Serikali yapinga mfungwa wa ugaidi kupewa dhamana

Mohamed alikata rufaa akidai kuwa na matatizo ya kiafya na changamoto za kifamilia.

avdeltanews@gmail.com

Serikali imepinga ombi la dhamana la mwanaume wa miaka 61 anayehudumia kifungo cha miaka 30 jela kwa kosa la ugaidi.

Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) anasema mfungwa huyo hastahili kuachiwa kwa dhamana akisubiri rufaa yake.

Mohamed Abdi Ali alipatikana na hatia mnamo Mei 22, 2025. Alihukumiwa Juni 19 mwaka huo kwa  kupanga na kusaidia shambulio la kigaidi katika hoteli ya Dusit D2, Nairobi.

Wakati wa shambulio hilo la mnamo Januari 15, 2019, watu 21 waliuawa.

Mohamed alikata rufaa wiki moja baada ya kuanza kutumikia kifungo, akidai kuwa na matatizo ya kiafya na changamoto za kifamilia.  

Kwa sababu hiyo, anataka kuachiwa kwa dhamana akisubiri rufaa hiyo isikilizwe.

Kupitia wakili wa mashtaka Duncan Ondimu, DPP aliambia Mahakama Kuu ya Kiambu kuwa makosa hayo ni mazito. Alisema yanahusiana moja kwa moja na ugaidi.

Ondimu alisema kumwachilia mfungwa kwa dhamana kutahatarisha usalama wa umma. Pia kutapunguza imani ya wananchi kwa mfumo wa haki.

Aliongeza kuwa haki itatendeka vyema zaidi ikiwa rufaa itasikilizwa kwa haraka.

"Hakuna sababu ya msingi ya kumpa dhamana. Hajaonyesha madhara makubwa atakayopata ikiwa ataendelea kukaa rumande," akasema.

Alisema ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma    iko tayari kusikiliza rufaa bila kuchelewa, japo haiioni kuwa na uzito.

“Mlalamishi hajaonyesha kuwa rufaa yake ina nafasi kubwa ya kushinda,” alisema Ondimu.

Mohamed aliwasilisha ombi hilo kwa hati ya dharura.

Kesi hiyo itatajwa tena tarehe 28 Februari 2026.

Mohamed Abdi Ali
Mohamed Abdi Ali aliyekata rufaa kifungo cha miaka 30 jela kwa kuhusika na shambulio la kigaidi katika hoteli ya Dusit D2, Nairobi. Picha/ODPP